Watumishi wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) wamepatiwa Mafunzo ya Maadili, Rushwa na Magonjwa yanayoambukiza na yasiyoambukiza ikiwa ni utaratibu wa Serikali kutoa Mafunzo hayo kwa watumishi wa Umma.

Mafunzo hayo yamefanyika leo Juni 27, 2024 katika ukumbi wa Prof. Abdulkarim Mruma ambapo watumishi wa taasisi hiyo wamepata fursa ya kuuliza maswali na kupatiwa majibu, kutoa ushauri na kupatiwa ushauri pamoja na kupima kwa hiari Virus vya UKIMWI (VVU).

Akizungumza Mwezeshaji wa Mafunzo hayo, Mchunguzi Mkuu wa Taasisi ya Kupambana na Rushwa (PCCB) Stephen Agwanda amesema lengo la Mafunzo hayo ni kuchochea utamaduni wa kufuata Miongozo, Sheria, Kanuni na Taratibu za Maadili katika Utumishi wa Umma ikiwemo Misingi nane ya Maadili ya Utumishi wa Umma na kuepuka Rushwa.

Aidha, Agwanda ametoa msisitizo kwa watumishi wa taasisi hiyo kuachana na utendaji kazi wa mazoea na badala yake kufanyekazi kazi kwa bidii na weledi kwa kufuata Miongozo, Sheria, Kanuni na Taratibu za Utumishi wa Umma.

Kwa upande wake, Mwezeshaji kutoka Ofisi ya Rais Utumishi Ally Ngowo ametoa wito kwa Watumishi wa GST kujijengea hali ya upendo, uaminifu na ushirikiano mahala pa kazi ili kuleta umoja na mshikamano na kuwataka watumishi hao kutoa huduma bora bila upendeleo na kuzingatia viwango.

Awali, Kaimu Mtendaji Mkuu wa GST Hafsa Maulid alifungua Mafunzo hayo na kuwataka watumishi wote kuwa wasikivu, kuuliza maswali, ufafanuzi na kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wawezeshaji.

Katika Mafunzo hayo, Stephen Agwanda kutoka Taasisi ya Kupambana na Rushwa (PCCB) ametoa mada ya Mapambano dhidi ya Rushwa mahala pa kazi, Dkt. Russel Halama kutoka Hospitali ya Mkoa wa Dodoma ametoa mada ya Magonjwa yanayoambukiza na yasiyoambukiza, Ally Ngowo kutoka Ofisi ya Rais Utumishi ametoa mada ya Maadili ya Utumishi wa Umma na Dkt. Baraka Edwin kutoka Hospitali ya Mkoa wa Dodoma ametoa mada ya Afya ya Akili.