Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Dkt. Anthony Diallo amewataka wakulima wa Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa kuzingatia kanuni bora za kilimo na ushauri wa wataalamu unaolenga kuwasaidia na kuwawezesha kuongeza tija kwenye kilimo chao.

Ametoa wito huo leo tarehe 21 April, 2024 alipotembelea kituo cha Mafunzo cha kampuni ya mbolea ya Yara na wakulima wa kijiji cha Ruaha Mbuyuni katika Wilaya ya Kilolo Mkoani Iringa kwa ziara ya Bodi na Menejimenti ya TFRA yenye lengo la kusikiliza changamoto za wadau wa tasnia ua mbolea na kuzitatua.

Akizungumza na wakulima wa maeneo hayo Dkt. Diallo amewataka kuongeza matumizi ya mbolea katika shughuli zao za kilimo kutakakopelekea kuongeza uzalishaji na kuinuka kiuchumi ukilinganisha na hali zao kiuchumi kwa sasa.

Aidha, ameeleza kuridhishwa na uwepo wa kituo cha mafunzo katika mji wa Ilula na kueleza kitasaidia katika kuhamasisha na kutoa elimu ya kilimo bora kwa wananchi na elimu ya matumizi sahihi ya mbolea ikiwemo.

Naye Mkurugenzi wa TFRA, Joel Laurent, ametambua mchango wa kampuni ya Yara na kuipongeza kwa juhudi kubwa ya kuelimisha wananchi wa Kilolo juu ya kilimo bora na kubainisha kinasaidia kukuza tasnia ya mbolea.

Amepongeza programu ya kuhamasisha watoto kushiriki kwenye kilimo na kueleza elimu hiyo inawajengea hali ya kupenda shughuli za kilimo hata watakapokuwa watu wazima.

“Programm kama hizi zinawaandaa watoto wetu kujua thamani ya kilimo kwenye maisha yao” Laurent aliongeza.

Aidha, ameeleza matamanio yake kuwa ni kuona wananchi wengi wakiongezeka kwenye mnyororo wa thamani/ biashara ya mbolea na kuongeza matumizi ya mbolea Ili kufikia Agenda 10/30: Kilimo ni Biashara.

Kwa upande wake, Afisa Kilimo wa Halmashauri ya Kilolo,Tumsifu Charles
Alitoa shukrani zake kwa kampuni ya mbolea ya Yara Tanzania Ltd kwa kuchukua sampuli za udongo katika vijiji 16 walikoanzisha mashamba darasa kwa ajili ya wakulima kujifunza na kuomba matokeo ya vipimo hivyo kurudishwa ili wakulima wanufaike kwa kutambua aina ya mbolea wanayotakiwa kutumia katika mashamba yao ilinkuondokana na kutumia mbolea kwa mazoea pasipo kupima afya ya udongo.

Ameeleza mpango wa ofisi yake wa kuanzisha programmu ya upimaji wa afya ya udongo katika kata na vijiji wanavyovisimamia kufuatia kupewa vifaa maalum kwa kazi hiyo kutoka Wizara ya kilimo na wadau wengine wa kilimo ambapo kwa sasa wanavifaa sita kwa kazi hiyo.

Naye, Donath Fungu Meneja wa Kilimo kwa Tanzaniq na Rwanda ameeleza kuwa kampuni yake hutoa mafunzo ya awali kwa wakulima kabla ya msimu ili kuwajengea uwezo wakati msimu wa kilimo unapowadia.

Amebainisha mpango wa kampuni wa kuajiri mtaalam wa kilimo kuanzia mwezi Mei, 2024 atakayehudumia wananchi watakaokua wakitembelea kituo cha mafunzo na kupewa huduma ya ushauri kwa muda wote wa kazi kuanzia saa 1.30 hadi saa 11 jioni.